10 Nov 2014


Kanisa halipaswi kuazima mitindo ya kiganga kuendesha huduma za maombezi. Mitindo ya kiganga ni pamoja na matumizi ya misamiati inayotumika kwenye anga za wapunga pepo, pamoja na kutumia
https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEjHWUgXFtO8xvkSY93ehC00laZieJ-eoQEnXvzibCAVYIV0iFCDWYA-laEuZT-4NuAl8nemSHthqLzIFKaeXFBlA3Jcoi8fEgXYRVMKUJF19cwjtx7YB95NSCH9pNrWbNnDQILFx7WjjWA/s1600/Askofu+Gamanywa+Gospel+Kitaa-1-1.jpeg
Askofu Sylvester Gamanywa.
uzoefu wa kiganga/kichawi mtu aliuokuwa nao kwenye ulimwengu wa giza na kuuleta katika huduma za kikanisa.

Hatari ya kuendekeza hii hali ni kuanguka kwenye mitego wa Ibilisi wa kujaribu kudhoofisha utendaji halisi wa nguvu za Roho Mtakatifu. Kumbuka Yule aliyekuwa Mchawi alivyotaka kununua uwezo/karama ya kuwekea watu ujazo wa Roho Mtakatifu ili autumie kwenye uzoefu wa kichawi aliokuwa kiufanya na kushangaza wengi huko Samaria. 

Kama sio Petro kupitia karama ya maarifa kumgundua hila zake si ajabu hata kama asingepokea fedha lakini angemkubalia kuifanya huduma ya kuombea watu Roho Mtakatifu na badala ya watu kujawa na Roho Mtakatifu wangejazwa “roho mtakafujo”!

Kwa hivi sasa, sio siri kwamba, tayari wako watu waliojiingiza katika huduma za maombezi kwa madai ya kuwafungua watu katika vifungo vya majini lakini miitndo inayotumika katika huduma hizo inaonesha dalili zote za “wapunga pepo” wanaotumia uzoefu wa kiganga/kichawi. Utawatambuaje? Ziko dalili za waziwazi kama Yesu alivyotabiri: “Mtawatambua kwa matunda yao.”:

Wanajiita watumishi wa Mungu lakini tabia na mienendo yao haina maadili ya utumishi wa Kristo. Wamejaa mizaha na utovu wa nidhamu usioambatana na utendaji wa huduma za kweli zinazomwakilisha Kristo katika utumishi. 

Kipaumbele sio kuwafundisha watu kumjia na kumjua Kristo na kuishi maisha ya utakatifu wa kweli. Wanachojali ni kuteneza wafuasi wengi wataoendelea kuwa na “imani tegemezi” kwao; badala ya kuwafundisha watu kumtegemea Kristo ambaye kimsingi ndiye mwenye mamlaka kamili ya kuwafungua na kuwaweka watu huru mbali na vifungo vya pepo wachafu.

Mara nyingi kipambele katika huduma ni kukusanya fedha kwa visingizio vya “jumbe zi kinabii” lakini zenye kuambatana na malipo kama kigezo cha kufunguliwa kwa wagonjwa na wenye pepo. Hii ndiyo ile ya Yule Simoni mchawi akiyeingiza suala la “kununua karama ya Mungu kwa mali” ili apate kuifanyia biashara katika maombezi

Kanisa halipaswi kupokea na kufanyia kazi
ushauri wa mapepo katika maombezi

Hili ni onyo kwa watumishi wa kweli wanaofanya huduma za maombezi, lakini pasipo kujua au kukusudia, wamejikuta wametumbukia katika mtego wa kutegemea taarifa zinazotolewa na mapepo yaliyowapagaa watu zinazodai sababu za kuwapagaa na nini kifanyike ili wawaachie waliowapagaa. 

Watumishi wa kweli wa Kristo, hawapaswi, kwa namna yoyote ile; kupokea na kufanyia kazi ushauri wa mapepo kama ndio mtindo na njia ya watu waliopagawa wapate kufunguliwa! 

Kwa kusema hivi sina maana kwamba pasiwepo kabisa mawasiliano na pepo wanapowapagaa watu. Ninachomaanisha ni kwamba wakati wa “mawasiliano na pepo”, ajenda kuu iwe ni “kuyakemea na kuyaamuru yatoke kwa mamlaka ya Kristo pasipo kutafuta kuwa na muafaka wa masharti ya mapepo”!

Uchunguzi na uzoefu nilioupata katika utumishi huu wa huduma za maombezi, ninao ushahidi wa kutosha kuthibitsha kwamba, sio wote wanaopagawa na pepo wakati wa maombezi hufunguliwa mara moja. Wengine huchukua muda kutokana na mfumo wa maisha wanayoishi, ufahamu duni wa Neno la Mungu, na utayari wa kujitoa kikamilifu kuishi maisha ya utakatifu kama yasemavyo maandiko. 

Kwa hiyo mapepo kupiga kelele na kuangusha watu chini wakati wa maombezi; kisichukuliwe kuwa kigezo pekee kwa wahusika wanafunguliwa. Kufunguliwa katika pepo kwa walio wengi ni mchakato ambapo wahusika wanatakiwa kutoa ushirikiano makini ikiwa ni pamoja na kuhimizwa kupokea wokovu wa Yesu Kristo, na utayari wa kupitia mafundisho makini ya Neno la Mungu na,  utayari wa kubadilika kitabia na mwenendo kama njia ya kufunguliwa kikamilifu.

Mungu alikwisha kutoa mamlaka
 ya kudhibiti uchawi kanisani 

Ni wakati wa kanisa sasa kurejea kwenye ufunuo wa kanisa la kwanza na kuwa na mamlaka ile ambayo Kristo aliwakabidhi mitume wake kama ilivyoandikwa:

“Akawaita wale Thenashara, akawapa uwezo na mamlaka juu ya pepo wote na kuponya maradhi. (LK. 9:1)"

Katika makala yaliyopita tulifunza kupitia maandiko haya kuhusu neno hili “Uwezo” kwa kiyunani linaitwa “Dunamis” lenye kumaanisha “nguvu ya kutenda miujiza ya uumbaji, au kuharibu nguvu za pepo wabaya”! Kwa hiyo, Yesu Kristo alipowapa wanafunzi wake “uwezo na mamlaka” juu ya pepo wote, maana yake aliwapa nguvu za kufukuza au kutoa pepo wabaya watoke ndani ya watu wengine bila mjadala!

Pia tuliwahi kujifunza kwamba Bwana Yesu alipoagana na wanafunzi wake, aliwaahidi kupokea hii nguvu ya “dunamis” mara tu Roho Mtakatifu atakapowashukia.

“Lakini mtapokea nguvu (dunamis) akiisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu kuanzia Yerusalemu, uyahudi wote, Samaria hata mwisho wa nchi.” (Mdo.1:8)

Mwisho kabisa, tunauoa utendaji wa mamlaka ya kupambana na kuvunja shughuli za uganga/uchawi kila mahali ambapo Injili ya Kristo ilipohubiriwa:

“Na watu wengi katika wale waliotumia mambo ya uganga wakakusanya vitabu vyao, wakavichoma moto mbele ya watu wote; wakafanya hesabu ya thamani yake, wakaona ya kwamba yapata fedha hamsini elfu.   Hivyo ndivyo neno la Bwana lilivyozidi na kushinda kwa nguvu.” (MDO 19:19, 20)

Maandiko haya yanashuhudia jinsi kanisa la kwanza lilivyotamba dhidi ya nguvu za uchawi na kuleta maelfu katika ufalme wa Mungu. Huu ndio uamsho unaohitajika makanisa wa kuendesha huduma za maombezi yenye mamlaka halisi ya nguvu za Roho Mtakatifu na kuonesha matokeo ya kufunguliwa kikamilifu kwa wote wanaomjia Kristo.

Haifai kabisa kanisa kuendelea kuongozwa na ushauri wa mapepo ambao huwajengea hofu waamini badala ya ujasiri wa kutoa pepo. Kumbuku Yesu Alisema “ishara hizi zitafuatana na hao waaminio kwa jina langu watatoa pepo” na sio “Hofu ya uchawi itafuatana na hao waaminio nao watapunga pepo”!?


Mwisho

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni